Pages

Sunday, June 30, 2013

Heshima ya mwanadamu katika utawala wa Imam Mahdi AS

Assalaamu Alaykum wapenzi wasikilizaji Warahmatullahi Wabarakatuh. Siku ya leo inasadifiana na siku aliyozaliwa mwokozi aliyeahidiwa, mtukufu Hujjatu Ibn al Hassan al Mahdi, Imamu wa Zama (Mwenyezi Mungu aharakishe kudhihiri kwake). Mtukufu huyo alizaliwa mwezi 15 Shaaban mwaka 255 Hijria katika mji wa Samarra kaskazini mwa Baghdad ya Iraq ya leo. Jina lake ni sawa na jina la Bwana Mtume SAW. Baba yake ni mtukufu Imam Hassan al Askari (AS) na mama yake ni Bibi mtukufu Nargis. Kwa mujibu wa hadithi mutawatir za Kiislamu na maandiko ya vitabu vitakatifu vya mbinguni, mtukufu Imam Mahdi (AS) atadhihiri katika Akhiruz Zaman na hivyo kuifanya ithibiti ahadi aliyotoa Mwenyezi Mungu.
Ataziondoa hatamu za utawala mikononi mwa madhalimu, na kwa amri ya Mwenyezi Mungu uendeshaji wa ulimwengu utakuwa mikononi mwake yeye mtukufu Mahdi, Qaaim wa Aali Muhammad SAW. Katika zama za utawala wa mwokozi huyo mwadilifu, dunia itashuhudia kurejea na kudhaminiwa heshima halisi na ya hali zote ya mwanadamu. Wapenzi wasikilizaji! Mbali na kukupeni mkono wa kheri na fanaka kwa mnasaba wa uzawa huu wenye baraka nakukaribisheni kusikiliza kipindi hiki maalumu ambacho kitazungumzia umuhimu wa heshima ya mwanadamu katika utawala wa mtukufu Imam Mahdi ( Ajjalallahu ta'ala farajahush sharif).
Mwanadamu ni mbora wa viumbe na mja aliyepewa izza na kutukuzwa na Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu Mtukufu amemuarifisha mwanadamu kuwa ni khalifa wake katika ardhi, na daraja na heshima yake kiumbe huyo imepandishwa na kuwa juu zaidi kuliko hata ya malaika walioamrishwa na Mola wamsujudie. Heshima ambayo ni hadhi na utukufu ni sehemu ya dhati ya maumbile ya mwanadamu. Katika baadhi ya aya za Qur'ani imeelezewa heshima na utukufu wa mwanadamu na ubora wake kulinganisha na viumbe wengine. Aya ya 70 ya Suratu Isra'a inasema:"Na hakika tumewatukuza wanaadamu, na tumewapa vya kupanda nchi kavu na baharini, na tumewaruzuku vitu vizuri vizuri, na tumewafadhilisha kwa fadhila kubwa kuliko wengi miongoni mwa tuliowaumba. Katika aya nyengine limetiliwa mkazo suala hili, kwamba vyote vilivyoko mbinguni na vilivyoko ardhini vimeumbwa kwa ajili ya mwanadamu, na yote haya ni ishara ya heshima, utukufu na ubora alionao kiumbe huyo kuwapita mahuluku na viumbe wengine wote wa ulimwengu. Lakini heshima na utukufu huo wa mwanadamu unatokana pia na kumtii kwake Mwenyezi Mungu. Kwa kumtii Mwenyezi Mungu Mtukufu, mwanadamu hufikia kwenye utukukaji wa kiroho na kutakasika na machafu yanayomdunisha na kumporomosha, utukukaji ambao humfikisha kwenye saada halisi ambayo ni maisha safi ya milele chini ya himaya ya rehma za Mwenyezi Mungu.
Wapenzi wasikilizaji, licha ya utangulizi wa Tangazo la Dunia la Haki za Binadamu kusisitiza juu ya heshima na adhama ya dhati aliyonayo mwanadamu lakini kwa masikitiko ni kwamba sio tu hakuna hatua za maana zilizochukuliwa kwa ajili ya suala hilo bali mwanadamu amezidi kuwa mbali na heshima yake halisi. Kwa sababu hiyo ili kuirejesha heshima ya mwanadamu yanahitajika mazingira ya msingi na kufanyika mageuzi ya kina. Leo hii watu wa dunia nzima, wa dini na kaumu mbalimbali wanamsubiri mwokozi wa kuja kuleta mageuzi hayo na kurejesha heshima na utukufu wa mwanadamu. Katika Uislamu, mwokozi huyo ni Hujjatu Ibn al Askari (AS) anayetoka katika kizazi kitoharifu cha Mtume wa mwisho wa Allah Nabii Muhammad SAW. Shakhsia ambaye atadhihiri ili kuja kuleta amani na uadilifu na kurejesha heshima halisi ya mwanadamu, na atafanya mapinduzi makubwa ndani ya majimui nzima ya uhusiano wa kijamii. Kwa kudhihiri mwokozi huyo vizuizi vya ndani na vya nje vinavyomzuia mwanadamu kufikia kwenye ukamilifu wa kiutu vitaondolewa na kupatikana mazingira ya kurejesha heshima ya kiumbe huyo.
Katika dini ya Uislamu Bwana Mtume Muhammad SAW pamoja na Ahlul Bayt wake wapenzi ambao ni waongozaji na waonyeshaji njia ya uongofu, kutokana na elimu waliyonayo juu ya Qur'ani na mafundisho yake matukufu waliipa umuhimu na mazingatio kamili nafasi, hadhi na daraja aali ya mwanadamu na walimuenzi na kumpa heshima kiumbe huyo. Kati ya watukufu hao, Imam Mahdi (Ajjalallahu ta'ala farajahush sharif) ambaye ni mjukuu wa Bwana Mtume na hazina na johari ya mwisho ya mbinguni iliyosalia katika zama zetu, mara baada ya kudhihiri ataelekeza juhudi na jitihada zake zote katika kumfikisha mwanadamu kwenye utukufu na ukamilifu ili kuihuisha na kuirejesha tena heshima na utukufu wa mwanadamu uliopotea katika zama za kughibu kwake. Kwa hivyo moja ya hatua, au tuseme hatua muhimu zaidi itakayochukuliwa na mtukufu huyo baada ya kudhihiri ni kuandaa mazingira yanayohitajika kwa ajili ya kurejesha heshima ya wanadamu. Zama za utawala wa Imam wa Zama AS zitakuwa zama za kuchanua vipawa na elimu za fani mbalimbali na kufikia kileleni elimu za wanadamu za kipindi chote cha historia. Elimu na maarifa yatapenya na kuenea ndani ya kila nyumba na kukita ndani ya akili na moyo wa kila mtu. Kutokana na kuja mwokozi wa ulimwengu ujinga na ujahili utatoweka na nafasi yake kuchukuliwa na elimu na maarifa, na mwanadamu ataipata tena johari yake ya heshima iliyokuwa imempotea. Ni wazi kwamba chimbuko la heshima ya mwanadamu linapatikana kwenye mafundisho halisi aliyotunukiwa mja huyo na Mola wake. Na kadiri mwanadamu atakavyonufaika na elimu na mafundisho hayo ndivyo atakavyopambika na heshima na fadhila za kiutu. Kuhusiana na suala hilo Imam Jaafar Sadiq (AS) amesema:"Elimu na utaalamu ni herufi 27. Yale yote ambayo Mitume wa Mwenyezi Mungu wamewaletea watu si zaidi ya herufi mbili tu, na hadi sasa watu hawajawa na utambuzi wa zaidi ya herufi mbili hizo. Lakini wakati Qaimu wetu atakaposimama herufi nyengine 25 zitadhihirika na kuenea kwa watu na zile herufi mbili nyengine zitaambatishwa na hizo ili kupatikana herufi zote 27". Hadithi hii inabainisha upandaji mkubwa na usio wa kawaida wa kiwango cha elimu katika zama za mapinduzi ya Imam Mahdi (AS); na tunajua kwamba kila mahali palipo na nuru ya elimu ya mbinguni wingu jeusi la hali ya kumdunisha na kumtoa thamani mwanadamu hutanduka na mwanga wa heshima ya utu hutanda na kuangazia nuru yake.
Ni hali ya kusikitisha kuona kwamba katika zama zetu hizi dhulma, ubaguzi na uchokozi wa majabari na wakoloni wa Magharibi umeidunisha heshima ya mwanadamu bali hata kuipoteza haki ya kuishi ya watu. Hali ya kuwa Mwenyezi Mungu anawataka wanadamu waheshimiane na kustahiana, na kila mmoja kuchunga haki za kimaada na za kimaanawi za mwenzake. Mbele yake Yeye Mola, mwanadamu anastahiki heshima na kutendewa uadilifu wa kweli na wala uhai wake wa hapa duniani usiwekwe rahani na kufanywa mhanga wa aina yoyote ile ya ukoloni, unyonyaji, dhulma na uonevu. Kwa hivyo miongoni mwa mambo yenye nafasi muhimu ya kuhuisha heshima na taadhima ya mwanadamu ni uadilifu. Kwa kuzingatia tafsiri na maana sahihi ya uadilifu ambayo ni kukiweka kila kitu katika mahala na nafasi yake kinachostahiki, kama uadilifu utatekelezwa kwa namna bora kabisa baina ya watu na baina ya jamii za watu bila ya shaka yoyote wanadamu watafikia kwenye daraja yao aali ambayo ni ya utu na ubinadamu kwa maana yake halisi. Katika wakati wa kudhihiri Imamu wa Zama uadilifu utatekelezwa katika masuala yote ya maisha ya mwanadamu, na watu wote watanufaika kiadilifu na neema za maumbile na atiya za Mola Mwenyezi. Aidha kutokana na kuenea uadilifu katika dunia heshima na utukufu wa watu wa mataifa, asili na rangi zote utadhaminiwa bila kuwepo ubaguzi na upendeleo wa namna yoyote.
Kwa hivyo utawala wa Imam Mahdi (AS) utakomesha dhulma na uonevu na kuhuisha malengo mema na matukufu ikiwemo heshima ya mwanadamu ulimwenguni kote. Kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, Imam atasimama na kufanikisha mapambano dhidi ya dhulma na kufungua ukurasa mpya katika historia ya mwanadamu na kumpa kiumbe huyo maisha na uhai mpya. Katika utawala wa Imam Mahdi (AS) mwanadamu atapata heshima yake halisi anayostahiki. Heshima ambayo imesimama juu ya msingi wa umaanawi na ukamilifu uliotukuka. Naye kama alivyo baba mwenye huruma atawafaidisha watu na wanadamu wote na neema hiyo ya heshima ya utu. Atakamilisha maadili ya akhlaqi njema, atakabiliana na vitendo vya uchupaji mipaka na kuwadunisha wengine, atawafanya waja wa Mwenyezi Mungu wapumue katika anga ya uhai mpya na atasimamisha haki na kuitokomeza batili.
Taqwa na kumcha Mungu ni moja ya mambo yanayoinua heshima ya wanadamu, suala lililo dhidi ya mwenendo wa kumwasi na kutomkhofu Mola. Ikiwa ndani ya nyoyo za watu na jamii zao utaenea na kuhanikiza uvundo wa maovu na kumwasi Mwenyezi Mungu na watu wakamsahau Mola katika mwenendo na matendo yao, bila ya shaka yoyote wataelekea kwenye hilaki na maangamizi, ambao ni muelekeo unaokinzana na harakati ya kufikia kwenye daraja na nafasi tukufu ya utu. Heshima na utukufu wa mwanadamu mbele ya Mwenyezi Mungu na vilevile ndani ya jamii unasimama juu ya msingi huu. Hii ikiwa na maana kwamba kila mtu mwenye kulinda mipaka ya Mwenyezi Mungu na kuchunga heshima ya fitra na maumbile yake na akajiweka mbali na machafu basi mtu huyo atakuwa na heshima na utukufu zaidi mbele ya Mola. Sehemu ya aya ya 13 ya Suratul Hujurat inasema: "Hakika aliye mtukufu zaidi kati yenu kwa Mwenyezi Mungu ni huyo aliye mchamngu zaidi katika nyinyi". Katika aya hii Mwenyezi Mungu anaashiria aina nyengine ya heshima na utukufu wa mwanadamu, heshima na utukufu ambao unapatikana kwa juhudi na idili na ambao una mfungamano imara na wa kudumu na taqwa na kumcha Mwenyezi Mungu.
Wapenzi wasikilizaji kwa mara nyengine tena ninakupeni mkono wa kheri na baraka kwa mnasaba huu adhimu wa kukumbuka kuzaliwa kwa mwokozi wa ulimwengu Imam Mahdi (AS). Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

No comments:

Post a Comment