Pages

Saturday, June 8, 2013

Jumuiya ya Nchi za Kiarabu yalalamikia siasa za kibaguzi za utawala wa Israel

Jumuiya ya Nchi za Kiarabu pamoja na taasisi na asasi nyingine za kutetea haki za binadamu zimetaka zichukuliwe hatua za haraka zenye shabaha ya kukomesha hatua za kijinai za utawala wa Kizayuni wa Israel kwenye ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu tokea mwaka 1948 na 1967. Taarifa iliyotolewa na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu 'Arab League'  imeeleza kuwa, maamuzi ya hivi karibuni ya utawala huo ghasibu ya kutaka kuwasilisha bungeni muswada wa kuundwa 'nchi ya Kiyahudi' umezitia wasiwasi nchi za Kiarabu. Kwa mujibu wa muswada huo wa kibaguzi, kwa akali Wapalestina milioni moja wanaoishi huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu yaani Israel wataondolewa  kwa nguvu  kwenye  makazi yao. Hivyo, Jumuiya ya Nchi za Kiarabu licha ya kulaani muswada huo wa kibaguzi, imesisitiza kuwa  kupitishwa kwake, kutahatarisha maisha ya raia wa Kipalestina wanaoishi katika maeneo yanayokaliwa kwa mabavu na Wazayuni tokea mwaka 1948.  
Weledi wa masuala ya kisiasa wanaeleza kuwa, kupitishwa kwa muswada huo kutahalalisha utawala wa Kizayuni wa Israel  kujitangazia taifa la Kiyahudi, jambo ambalo litapelekea kuporwa zaidi ardhi za Wapalestina na kupewa Mayahudi. Aidha, iwapo muswada huo utapitishwa na kuwa sheria, lugha ya Kiebrania itakuwa lugha pekee rasmi itakayotambulika rasmi huko Israel, na hivyo kufutwa kabisa lugha ya Kiarabu ambayo pia ni lugha inayotambuliwa na utawala huo. Benjamin Netanyahu Waziri Mkuu wa utawala wa Israel alipendekeza mpango wa kuundwa serikali mbili, za Kiyahudi na Kipalestina mwaka 2010. Kwa mujibu wa mpango huo, kwa mara ya kwanza tokea Wazayuni wazikalie kwa mabavu ardhi za Palestina kwa zaidi ya miongo sita sasa, utawala wa Israel utaweza kujitangazia taifa la Kiyahudi na hivyo kuwafukuza Waarabu wa Kiapalestina wanaoishi huko. Mara kadhaa utawala wa Kizayuni wa Israel umekuwa ukidai kuwa unaafiki kuundwa serikali huru ya Palestina katika ardhi zilizokaliwa kwa mabavu mwaka 1967, amma wimbi la ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni kwenye ardhi za Palestina, unaonyesha kinyume na madai hayo.  Umoja wa Mataifa umetoa makumi ya maazimio dhidi ya utawala wa Israel ya kuutaka utawala huo ghasibu uondoke bila ya masharti kwenye ardhi unazozikalia kwa mabavu tokea mwaka 1967. Kwa mujibu wa azimio nambari 194 la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, baraza hilo lilipitisha azimio lililowapa Wapalestina haki ya kurejea kwenye makazi yao yaliyokaliwa kwa mabavu na Wazayuni mwaka 1948. Kwa minajili hiyo, kuundwa serikali ya Kiyahudi, siyo tu kunakinzana na maazimio ya Umoja wa Mataifa, bali ni dhihirisho la wazi la ubaguzi unaotekelezwa na utawala huo dhidi ya Wapalestina. Kwa maana nyingine, Wapalestina baada ya miaka kadhaa ya kuwa wakimbizi na ardhi zao kukaliwa kwa mabavu, hivi sasa wanakabiliwa na jinamizi jingine la siasa za ujenzi wa vitongoji na mpango wa kuundwa taifa la Kiyahudi. Hii ndio maana  Jumuiya ya Nchi za Kiarabu ikaziomba Umoja wa Mataifa na taasisi za kutetea haki za binadamu ziingilie kati na kuzuia siasa za kutaka kujitanua utawala wa Israel katika ardhi za Wapalestina.

No comments:

Post a Comment