Pages

Saturday, June 8, 2013

Nabii wa Rehma

Amani ya Allah, rehma na baraka zake ziwe juu yenu wapenzi wasikilizaji. Kwa furaha na moyo mkunjufu nakukaribisheni kujiunga nami tena katika sehemu hii ya 19 ya kipindi hiki kinachodondoa machache kati ya mengi  yaliyosemwa na wasomi na shakhsia mbalimbali wasio Waislamu lakini wenye insafu kuhusu Mtume wa Mwisho wa Allah, mbora wa viumbe na Nabii wa rehma Muhammad SAW. Ni matumaini yangu kuwa mtaendelea kuwa nami hadi mwisho wa kipindi kusikiliza niliyokuandalieni kwa leo.
Wapenzi wasikilizaji, katika sehemu 18 za mfulululizo huu wa kipindi cha "Yaliyosemwa na Wenye Hekima Kuhusu Nabii wa Rehma" tumejaribu walau kwa muhtasari kudondoa na kuchambua mitazamo ya wanafikra wa Magharibi kuhusu nabii wa rehma Muhammad SAW.
Katika kipindi chote cha historia yake, kutokana na kukosa kuwa na uelewa sahihi juu ya Uislamu na Mtume wake mtukufu, Ulimwengu wa Magharibi umeifanyia dhulma kubwa dini hiyo na nabii wake wa rehma. Hata hivi sasa pia huko barani Ulaya na katika Ulimwengu wa Magharibi kwa ujumla zingali zinasikika kauli na kushuhudiwa maandishi na harakati za kiadui, chuki na taasubi dhidi ya Bwana Mtume Muhammad SAW na dini tukufu ya Uislamu aliyokuja nayo. Ryland, mwandishi wa kitabu kiitwacho" Dini ya Wafuasi wa Muhammad" anasema hivi katika kitabu chake hicho:"Si jambo lenye shaka yoyote kwamba lau kama itakuwepo dini moja tu katika ardhi ambayo maadui zake wameielezea kwa sura mbaya zaidi na kuonyesha chuki dhidi yake basi dini hiyo ni Uislamu", mwisho wa kumnukuu.
Bila ya shaka uadui uliopo hivi sasa dhidi ya Uislamu na nabii wake wa rehma, zaidi unafanywa na watu wasio na hekima na wanaofanya hivyo kwa sababu zao maalumu. Kumtusi na kumvunjia heshima Bwana Mtume kunakofanywa na Wamagharibi, baadhi ya wakati kumesababisha misuguano mikali baina ya Magharibi na Ulimwengu wa Kiislamu. Pamoja na hayo ukweli wa mambo uko namna nyengine kabisa kwa mtazamo wa watu wenye hekima na wanaohukumu mambo baada ya kuyaangalia kwa jicho la haki na insafu. Watu wengi wenye hekima katika Ulimwengu wa Magharibi, kutokana na kuwa na moyo wa insafu na kuitumia neema ya hekima na tafakuri wamekuwa na mtazamo chanya mno kuhusiana na shakhsia safi na iliyotakasika ya nabii wa rehma Muhammad SAW na wameisifu na kuienzi kazi adhimu iliyofanywa na mtume huyo mteule wa Mwenyezi Mungu. Pengine ni kwa sababu hiyo ndio maana yeye Bwana Mtume SAW amesema:" Hakuna kitu kizuri zaidi kama hekima".
Wasikilizaji wapenzi katika sehemu hii ya 19 na itakayofuatia ya 20 ambayo itakuwa ndio ya mwisho ya kipindi hiki tutajaribu kudondoa maneno yaliyosemwa na baadhi ya wanafikra wengine wa Magharibi kuhusu nabii wa rehma Muhammad SAW. Hao ni watu ambao wanakiri waziwazi kuwa katika giza totoro la historia, Muhammad SAW alichomoza mithili ya nyota ing'arayo katika upeo wa anga; na katika zama ambapo ujahili na khurafa vilikuwa vimewagubika wanadamu mtukufu huyo aliutangazia ulimwengu wito wa tauhidi na uokovu.
Barthélemy-Saint-Hilaire ambaye ni mmoja wa wanahistoria wa zama hizi anasema:" Mtume wa Uislamu aliwashinda na kuwazidi watu wote wa zama zake kwa akili na fahamu, kumwabudu Mungu, huruma na insafu. Utawala ambao aliuasisi ulijengeka juu ya msingi wa maadili na fadhila za kiakhlaqi, na dini aliyoitangaza ilikuwa ni neema kubwa kwa watu walioikubali na kuifuata".
Jean-Jacques Rousseau, mwanafikra mkubwa wa Kifaransa ambaye aliishi katika zama moja na Voltaire ambaye tulizungumzia fikra na mitazamo yake kuhusu Bwana Mtume katika vipindi vilivyopita, yeye anaizungumzia busara na hekima ya kisiasa ya nabii huyo wa rehma kwa kusema:"Mtume Muhammad alikuwa na ufahamu sahihi kabisa kuhusu utawala na akaufanya kuwa na hali moja na sawa mfumo wake wa kisiasa na mfumo wake wa kidini; na kwa muda wote ambao muundo na thamani za utawala wake viliendelea kuwepo katika zama za viongozi waliokuja baada yake, utawala ulikuwa ukiendeshwa vizuri na ulikuwa na nidhamu na uwiyano kamili".
Kati ya wanafikra wa Magharibi yamkini ikawa hakuna mtu aliyezungumzia vizuri zaidi sifa ya kuwa hai, kwenda na zama na wakati na kukamilika kwa kila kitu dini tukufu ya Uislamu kama alivyofanya George Bernard Shaw. Yeye alitabiri kwa kusema: "Katika muda si mrefu ujao dini ya Uislamu itakuwa dini ya ulimwengu na itakayoenea kila mahala. Walimwengu wanataka kuwa na maisha yaliyojengeka juu ya msingi wa akili na umaanawi lakini mtu hatoweza kuupata umaanawi huo katika dini nyenginezo ghairi ya Uislamu. Shaw anaendelea kufafanua kwa kusema:" Kwa mawazo yangu Uislamu ndio dini pekee yenye sifa zinazoweza kuvutia mabadiliko ya namna tofauti na kuafikiana na hali na sura za kila zama na wakati. Mimi nimetabiri kuhusu dini ya Mtume Muhammad kwamba dini yake itaweza kukubalika katika Ulaya ya kesho, kama ambavyo kukubalika kwake kumeshaanza kuonekana katika Ulaya ya leo". Mtafiti huyu mashuhuri wa Uingereza ameendelea kumzungumzia nabii wa rehma Muhammad SAW kwa kuandika hivi:" Muhammad ndiye mtume mkubwa zaidi kuliko Mitume wote. Laiti kama angetawala katika ulimwengu wa leo angeondoa vinyongo vyote na kutatua matatizo yote ya wanadamu moja baada ya jengine kwa ishara tu ya kidole chake cha akili na hekima. Mimi ninaitakidi kuwa dini ya Muhammad (SAW) ni dini pekee inayofaa kwa ajili ya zama zote za maisha ya mwanadamu na yenye uwezo wa kukivutia kila kizazi".
Wapenzi wasikilizaji, kutokana na kumalizika muda uliotengwa kwa ajili ya kipindi hiki sina budi kukomea hapa na kukuageni hadi juma lijalo inshallah tutakapokutana tena katika mfululizo mwengine wa kipindi hiki. Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.

No comments:

Post a Comment