Pages

Tuesday, June 18, 2013

Magonjwa ya Uasherati (Sexual Transmitted Diseases)

Ahlan wa Sahlan wapenzi wasikilizaji na ni wasaa na wakati mwingine wa kuwa nanyi tena katikakipindi cha Ijue Afya Yako.Baada ya kumaliza kuzungumzia uzito wa kupindukia na namna ya kupunguza uzito na tumbo, tutaendeleza kipindi chetu kwa kuyaelezea magonjwa mbalimbali ya zinaa au kwa kimombo sexually transmitted diseases (STD).Natumai kuwa mtakuwa nami hadi mwisho wa kipindi, karibuni kunitegea sikio.
Kati ya magonjwa yanayoathiri watu wengi sana duniani ni magonjwa ya zinaa. Haya ni magonjwa yanayoambukizwa kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine kupitia vitendo vya ngono. Vitendo hivi vya ngono vinaweza kuwa kujamiana, kubusiana, vitendo vya ngono kwa kutumia mdomo (oral- genital sex), kujamiana kupitia njia ya haja kubwa (anal sex) iwe kwa mwanamume na mwanamke au kati ya wanaume wenyewe na hata wale wanaotumia vifaa vya kufanyia ngono (vibrators). Magonjwa ya zinaa huathiri sana watu walio na umri wa kati ya miaka 15 hadi 24 lakini pia yanashuhudiwa kwa wingi kwa watu wengine walio na umri wa chini au zaidi ya huu niliotaja. Kuna magonjwa ya zinaa zaidi ya ishirini yanayotambulika duniani, yakiemo haya:-

Kisonono (Gonorrhoea) au "Gono" kama wengi wanavyopenda kuuita kwa kifupi, Chlamydia, kaswende (Syphillis), ugonjwa wa zinaa unambukizwa na virusi vya HPV au  Human Papilloma Virus, Ukimwi yaani Upungufu wa Kinga mwilini Au HIV/AIDS, Hepatitis B, C, A, ugonjwa wa zinaa unasambabishwa na virusi aina ya Herpes  au Herpes virus, Trichomoniasis, ugonjwa wa zinaa unambukizwa na bakteria au Bacteria Vaginosis, chawa kwenye nywele za sehemu za siri na Chancroid. Tunawaahidi wapenzi wasikilizaji kuwa tutajaribu kuyachambua na kuyaelezea magonjwa hayo katika vipindi vyetu vijavyo ili tuweze kuyajue vyema magonjwa hayo na kujiepusha nayo, na wale ambao kwa bahati mbaya wanasumbuliwa na magonjwa hayo waweze kuyatibu na kujiepusha kuwaambukiza wengine, lengo kuu likiwa ni kuimarisha afya ya jamii kwa ujumla.
Ijapokuwa magonjwa yote ya zinaa huathiri jinsia zote, lakini baadhi ya magonjwa hayo huwa na madhara zaidi kwa wanawake. Hii ni kwa sababu pale mwanamke mjamzito anapokuwa na ugonjwa wa zinaa, baadhi ya magonjwa hayo huweza pia kumuathiri mtoto atakayezaliwa.

Tunapaswa kufahamu kuwa magonjwa mengi ya zinaa au STDs yanatibika lakini kuna baadhi ambayo hayana tiba ya uhakika kama vile Ukimwi, HPV, na Hepatitis B na C. Pia baadhi ya magonjwa hayo yameanza kuwa sugu na kutosikia tiba kutokana na matumizi holela ya dawa za antibiotics magonjwa hayo ni kama vile kisonono.  Ingawa tutazungumzia magonjwa hayo moja moja lakini mara nyingi sababu zinazopelekea watu kupatwa na magonjwa ya zinaa hufanana, kwa hivyo hapa tutaashiria kwa ujumla visababishi vya magonjwa ya zinaa:-

Vitendo vya ngono kama tulivyoashiria hapo awali.Kuanza vitendo vya ngono mapema au wakati wa umri mdogo.Kuwa na wapenzi au washiriki wengi wa ngono, tukimaanisha  kufanya ngono na watu tofauti.Kufanya ngono zisizo salama au ngono zembe.Maambukizi kupitia michibuko au sehemu zilizokatika kwenye ngozi kwa kugusana na majimaji ya aina yoyote yanayotoka kwa mtu mwenye ugonjwa wa zinaa kama damu, mate na kadhalika. Hii inaweza kutokea bila mtu kujua kwani mara nyingi dalili za magonjwa ya zinaa huwa hazionekani mapema kwa wanawake na hata baadhi ya wanaume. Tunapenda kukumbusha nukta hii kuwa, watu wengi huhisi kuwa, kitendo cha kubusiana ni salama, lakini si kama wanavyofikiria kwani baadhi ya magonjwa kama kaswende, herpes na mengineyo, yanaweza kuambukizwa kupitia njia hii. Kondomu au mipira ya kiume husaidia kupunguza maambukizi ya magonjwa ya zinaa kama gono, chlamydia na kadhalika lakini sio kinga muafaka ya magonjwa ya zinaa kama vile kaswende, genital herpes na genital warts.

Wasikilizaji wapenzi tutaanza kuzungumzia ugonjwa wa kisonono au gonorrhea kwa kimombo huku tukiendelea kuyachambua magonjwa mengineyo katika vipindi vinavyofuata.
Kisonono ni nini? Kisono ni ugonjwa kati ya magonjwa ya zinaa unaosababishwa na bakteria aina ya Neisseria gonorrhoeae, bakteria ambao hukua na kuzaliana kwa haraka katika sehemu zenye unyevunyevu na joto mwilini kama kwenye shingo ya kizazi kwa wanawake (cervix), mirija ya kupitisha mkojo au mbegu za kiume (urethra), mdomoni na kwenye puru au rectum. Maambukizi mengi kwa wanawake hutokea kwenye shingo ya kizazi. Asilimia 75 ya ugonjwa wa gono huwapata watu wenye umri wa kati ya miaka kati 15 hasi 29, ambapo wanawake walio katika umri wa miaka 15  hadi 19 na wanaume walio katika umri wa miaka 20  hadi 24 wako kwenye hatari zaidi ya kupata ugonjwa huu.Hii inaonesha kuwa ugonjwa wa kisonono huwapata zaidi vijana.
Je, Ugonjwa wa gono huambukizwa vipi? Ugonjwa huu huambukizwa kupitia vitendo vya ngono kutoka kwa mtu utakayejamiiana naye kupitia uke, njia ya haja kubwa na kupitia mdomo. Ugonjwa huu unaweza kujitokeza kwenye sehemu za siri, kwenye mdomo na kwenye puru au recktamu. Pia mama mjamzito mwenye kisonono anaweza kumuambukiza mwanaye wakati wa kujifungua. Licha ya ugonjwa wa gono kuonekana sana miongoni mwa vijana, pia unaonekana kwa watu wenye maisha duni kiuchumi, watu wanaoishi mijini, watu wenye asili ya Afrika na watumiaji madawa ya kulevya.

Wasikilizaji wapenzi mnategea sikio Idhaa ya Kiswahili Sauti ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, na kama ndio kwanza unafungulia redio yako kipindi kilichoko hewani ni cha Ijue Afya Yako. Tuendeleze kipindi chetu kwa kuelezea dalili za ugonjwa wa kisonono. Sio mara zote kisosnono huonyesha dalili, lakini kwa kawaida dalili za ugonjwa huo huanza kujitokeza kuanzia siku ya 2 hadi ya 7 baada ya mtu kupata maambukizi ya ugonjwa huo na huweza kuchelewa kuonyesha dalili hasa kwa wanawake. Dalili za ugonjwa huo ni kama zifuatazo:-
Kwa wanaume ugonjwa wa kisonono husababisha kuhisi kama kichomi wakati wa kukojoa (burning sensation). 2) Kutokwa na majimaji ya njano, meupe au ya kijani kwenye uume yanayoambatana na maumivu makali sana. 3) Wakati mwingine kuhisi maumivu au kuvimba kwa korodani (swollen testicles). 4) Maambukizi yakiwa kwenye puru (rectum) huambatana na maumivu wakati wa kujisaidia haja kubwa, kuwashwa sehemu za haja kubwa, na hata haja kubwa inaweza kutoka ikiambatana na damu, hili hutokea kwa wanaume na wanawake pia.

Dalili za ugonjwa wa gono kwa wanawake huwa si nyingi na wanawake wengi huwa hawaonyeshi dalili zozote. Lakini dalili wanazoonyesha wanawake ni kuhisi maumivu au kuhisi kichomi wakati wa kukojoa, kuongezeka kutokwa majimaji ukeni, majimaji ambayo ni ya njano au yaliyochanganyika na damu. Kutokwa damu kabla ya hedhi kufikia wakati wake wa kawaida, kutokwa na damu baada ya tendo la ndoa, kuhisi kichefuchefu, homa na kutapika. Inafaa kuashiria hapa kuwa ugonjwa wa kisonono kwa wanawake unaweza kusababisha uvimbe katika fupanyonga au pelvic inflammatory disease, ugonjwa mbao huleta matatizo wakati wa ujauzito na kusabisha ugumba. Hivyo, wanawake wanaohisi dalili tulizozitaja wanapaswa kumuona daktari mapema ili wafanyiwe vipimo na iwapo wana ugonjwa wa kisonono basi watibiwe haraka.

Na tunahitimisha kipindi chetu cha leo kwa kueleza vipimo vya ugonjwa wa kisonono. Moja ya vipimo vya gono ni kile kinachoitwa kitaalamu 'swab for culture'. Kipimo hiki hufanyika kwenye maabara kwa kupandikiza bakteria baada ya kufuta sehemu za siri kwa kutumia pamba au swab ili kuona kama kuna bakteria wanaosababisha gono. Kipimo kingine ni PCR au Polymerase Chain Reaction ambacho ni cha kuangalia vinasaba au DNA ya bacteria kutoka kwa mgonjwa. Kipimo hiki cha damu ni ghali. Baada ya mgonjwa kupimwa na kuthibitika kwamba ana ugonjwa wa kisonono, matibabu hufuata.
Lakini kwa kuwa muda tuliotengewa kipindi cha afya umetutupa mkono, tunaahidi kuzungumzia matibabu ya ugonjwa wa kisonono katika kipindi chetu kijacho. Hadi wiki ijayo apendapo Allah, tujitahidi kutunza afya zetu.

No comments:

Post a Comment