Pages

Saturday, June 22, 2013

Uislamu Chaguo Langu

Assalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh wapenzi wasikilizaji.
Kinyume na juhudi kubwa za vyombo vya habari vinavyofungamana na Wazayuni ambavyo vinaupiga vita Uislamu kwa kila njia, bado tunashuhudia kuongezeka idadi ya watu wanaovutiwa na kuukumbatia Uislamu kote duniani.
 Machi 30 mwaka 2008, taarifa ya makao makuu ya Kanisa Katoliki Duniani, Vatican ilisema kuwa Uislamu umeipita Kanisa Katoliki kwa wingi wa wafuasi kote duniani. Katika taarifa yake, serikali ya Vatican ilisema njama za watawala wa nchi za Magharibi kuharibu jina la Uislamu ni moja ya sababu za kuenea Uislamu miongoni mwa Wamagharibi. Vatican ilikiri kuwa kwa mara ya kwanza katika historia, Uislamu umechukua nafasi ya kwanza kwa mtazamo wa idadi ya wafuasi. Kwa hakika katika miaka ya hivi karibuni,  wakaazi asili wa Ulaya na Amerika Kaskazini ambao ni wafuasi wa Ukristo na dini nyinginezo wamekuwa wakisilimu kwa wingi pamoja na kuwa serikali za kipepari na kiliberali katika nchi hizo zimewekeza kiasi kikubwa cha fedha katika kueneza chuki dhidi ya Uislamu.

Bi. Melissa Carter ni Mmarekani aliyesilimu ambaye anafafanua kuhusu suala hili kwa kusema: "Hivi sasa Uislamu unaenea kwa kasi kubwa sana na jambo la kuvutia ni kuwa aghalabu ya wanaosilimu ni wasomi na hili linatokana na kuwa Uislamu unaenda sambamba na elimu na sayansi. "Katika makala yetu ya leo ya "Uislamu Chaguo Langu" tutamuangazia Mmarekani huyu aliyesilimu. Karibu kujiunga nami hadi mwisho wa kipindi.


Melissa Carter  ni mtafiti na mtengeneza filamu katika kituo maarufu cha Hollywood nchini Marekani. Mvuto wa lugha ya Kifarsi ndio uliopelekea kuibuka mabadiliko makubwa katika mkondo wake wa maisha kwani aliweza kuujua Uislamu kupitia lugha hii. Anafafanua kwa kusema: "Kabla ya kusilimu nilikuwa nikifanya utafiti kuhusu lugha ya Kifarsi kwa sababu nilivutiwa sana na Iran na utamaduni wake. Nilikuwa nikisoma na kutwalii vitabu vya malenga mashuhuri Wairani kama vile Sa'adi, Molana na Hafiz. Kutokana na kuwa mashairi ya malenga hawa wakubwa yalikuwa na maduhui za mafundisho ya Kiislamu na Irfani, niliweza kuujua Uislamu kupitia vitabu vya malenga hawa.  Aidha nilisoma tafsiri ya Qur'ani na kuvutiwa sana na niliiona kuwa ya kimetafizikia. Nilikuwa sijapata kuona elimu kamili kama hiyo Marekani. Kwa mtazamo wangu, Qur'ani  inamletea mwanaadamu shauku na nuru." Bi. Melissa Carter anaendelea kusema: "Niliamua kuelekea Iran ili kufanya utafiti  zaidi kuhusu vitabu nilivyokuwa nimevisoma. Niliweza kujuana na watu ambao walinipa maelezo mazuri katika vikao vilivyodumu masaa mengi. Niliweza kufahamu kuwa Uislamu ni dini adhimu iliyojaa mafunzo yenye thamani za juu jambo ambalo halipatikani katika dini nyinginezo. Baada ya utafiti wangu huo niliamua kuwa Mwislamu.  Ingawa jamii na baadhi ya marafiki zangu walikuwa na mtazamo mbaya kuhusu uamuzi wangu, lakini baba yangu ambaye alikuwa kasisi wa Kikristo hakupinga uamuzi wangu. Hata aliisoma Qur'ani na baada ya hapo akaniambia hana tatizo na uamuzi wangu wa kusilimu."


Adhana ni njia ya mawasiliano ya Allah SWT. Ni mukhtasari wa fikra takasifu za Uislamu; fikra ambazo huakisiwa kupitia maneno mazuri na ya kuvutia. Adhana ni njia ya mawasiliano ya Allah SWT ambayo huanza na kumalizika kwa tamko tukufu la 'Allah'. Adhana huanza kwa Allahu Akbar na kumalizika kwa La Ilaha Ila Allah. Kuna ujumbe muhimu katika mwanzo na mwisho wa adhana. Kati ya ujumbe tunaopata hapo ni kuwa dunia hii imetokana na Allah SWT na marejeo ya kila kitu ni kwake Yeye. Yeye pekee ndiye Muumba, Mwenye Mulki na Mola Muumba. Kwa hivyo itikadi yoyote ambayo marejeo yake si Allah SWT ni itikadi isiyo na thamani wala maana. Mmarekani aliyesilimu Bi. Melissa Carter pia alivutiwa na kuathiriwa kwa kiasi kikubwa na maneno ya adhana yenye uzito mkubwa. Anafafanua kwa kusema: "Nilivutiwa sana niliposikia sauti ya Adhana. Mara ya kwanza niliposikia Adhana nilikuwa safarani Dubai. Machozi yalinitoka baada ya kusikiliza adhana na nilihisi kana kwamba moyo wangu ulikuwa umepata umaanawi mkubwa na kwa muda wa siku nzima nilikuwa nikitafakari kuhusu Allah SWT. Adhana ni nembo ya kumkumbusha mja amkumbuke Allah SWT kwani mwanaadamu ni mwenye kughafilika. Muumba wa mwanaadamu anavijiua viumbe vyake, anajua mahitaji yetu na hivyo ametuwekea wazi njia ya kumkumbuka katika Uislamu ili tuelekee katika njia nyoofu."
Uislamu ndiyo dini kamilifu zaidi ya Mwenyezi Mungu. Dini hii ina mtazamo wa kuhimiza sayansi na elimu. Uislamu unamtaka mwanaadamu atafute elimu na maarifa na ajitolee muhanga katika njia ya kupata elimu. Hii ni kwa sababu kadiri elimu yenye nia njema inavyoongezeka, mja hujikurubisha zaidi kwa Mwenyezi Mungu. Kwa mujibu wa mafundisho ya Kiislamu, elimu na dini ni mambo ambayo yanaenda sambamba. Bi. Carter naye pia baada ya kusilimu aliweza kudiriki kikamilifu uhusiano baina ya elimu na dini katika Uislamu. Kuhusu hilo anasema: "Uislamu ni dini ya elimu na maarifa. Kabla ya kuujua Uislamu nilidhani kuwa dini hii inahusu kumuamini Mwenyezi Mungu tu lakini punde baada ya kusilimu ulimwengu mpya ulifunguka mbele yangu. Nilianza kutazama taaluma kama vile fizikia, kemia na biolojia kwa mtazamo wa Kiislamu. Kwa maoni yangu Uislamu ni dini ya kimantiki kabisa na ambayo imeangazia kila sehemu ya maisha."
Tokea mwanzo wa kudhihiri Uislamu maadui walikuwa na wasi wasi kuhusu kuenea dini hii tukufu. Walikuwa wakieneza propaganda kuwa Uislamu unaenea kwa upanga na nguvu za kijeshi. Lakini kinyume na madai hayo Uislamu ulikuwa umekita mizizi katika nyoyo za watu.


Hivi sasa watu wengi katika nchi za Magharibi hasa Mareknai wameukubali Uislamu baada ya kufanya uchunguzi na utafiti wa kina kuhusu dini hii ya Allah SWT.  Bi. Carter anafafanua zaidi kuhusu hili kwa kusema: "Watu wengi Marekani huvutiwa sana na Uislamu baada ya kupata maelezo mafupi tu sahihi kuhusu dini hii tukufu. Wamarekani wana hamu sana ya kujua historia ya Uislamu na kwa mfano wanaposoma historia ya Uislamu barani Ulaya na namna Waislamu walivyofika barani humo hufikia natija kuwa kuna upotoshaji mkubwa kuhusu Uislamu." Bi. Carter anaongeza kuwa:  "Nchini Marekani kuna watu wengi ambao wanafungamana na dini zao na wengi wanasema misingi ya Uislamu inakaribiana na utamaduni wao. Katika upande mwingine Uislamu pia ni dini ya mantiki na kila ambaye anachunguza kwa makini misingi yake, bila shaka huvutiwa na dini hii. Lakini kutokana na propaganda shadidi dhidi ya Uislamu inakuwa vigumu sana kuzungumzia Uislamu. Pamoja na masaibu hayo yote tunajitahidi kueneza Uislamu na watu wengi wanasilimu." Bi. Carter anaendelea kusema: "Nilikuwa na rafiki yangu aliyekuwa na mtazamo mbaya sana kuhusu Uislamu. Siku moja nilimpa kitabu cha Nahjul Balagha cha Imam Ali AS kisha baada ya muda akarejea kwangu na kutamka maneno haya: "Ali ni shakhsia mkubwa sana na sijawahi kusoma kuhusu shakhsia mithili yake". Kila mwanaadamu huhitajia kigezo mashani na kila harakati huwa kamili pale inapokuwa na kiongozi. Baada ya kuja Iran, Bi. Carter alimtambua Ayatullah Khamenei kama kiongozi wake mwenye uwezo na thamani za juu. Anafafanua zaidi kwa kusema: "Ninampenda sana Kiongozi wa Iran. Ni kiongozi wa harakati na mapinduzi muhimu sana. Ni kiongozi anayewasaidia wananchi ili wafikie lengo lililoainishwa. Leo tatizo la harakati za Kiislamu na Harakati ya Kuikalia Wall Street Marekani (Occupy Wall Stree) ni kuwa harakati hizo hazina kiongozi mwenye kutoa miongozo kama kiongozi wa Iran." Hivi sasa Bi. Melissa Carter anajitahidi kutengeneza filamu kwa msingi wa mafundisho ya Kiislamu. Anasema anataka kutekeleza majukumu yake kama Mwislamu hasa kueneza Uislamu kote duniani. Aidha Bi. Carter anajitahidi kukabiliana na fikra potofu za Hollywood kwa kutengeneza filamu ambazo zitauarifisha Uislamu kwa njia sahihi.

No comments:

Post a Comment