Pages

Saturday, June 8, 2013

Jumapili 29 Rajab 1434

Siku kama ya leo miaka 45 iliyopita, alifariki dunia Ayatullah Sayyid Muhammad Hassan Ilahi Tabatabai, mmoja wa maulamaa na wataalamu wa elimu ya irfani. Sayyid Muhammad Twabatwabai alizaliwa mjini Tabrizi kaskazini mwa Iran, mwaka 1325 Hijiria. Akiwa na miaka 19 alielekea mjini Najaf, Iraq akiwa na kaka yake mkubwa Allamah Muhammad Hassein Tabatabai na kupata kusoma elimu ya dini mjini hapo. Baada ya kutabahari katika elimu ya Kiislamu alirejea eneo alikozaliwa la Tabriz na kujishughulisha na kuwalea wanafunzi.

Miaka 128 iliyopita mwafaka na leo vikosi vya Ujerumani viliivamia nchi ya Magharibi mwa Afrika ya Togo. Katika kipindi hicho mwambao wa nchi hiyo ulikuwa umegeuzwa na watu wa Ulaya kuwa eneo muhimu la biashara. Nchi ya Togo iliendelea kuwa chini ya wakoloni wa Ujerumani, hadi kipindi cha Vita vya Kwanza vya Dunia. Baada ya Wajerumani kuondoka nchini Togo, Ufaransa na Uingereza ziliikalia tena kwa mabavu nchi hiyo. Hatimaye mwaka 1960 Togo iliweza kujipatia uhuru wake.
Siku kama ya leo, miaka 555 iliyopita alifariki dunia huko mjini Aleppo, Syria Shamsud-Din, faqihi na mfasiri mkubwa wa Waislamu wa zama hizo. Shamsud-Din alisoma elimu ya fikihi na tafsiri ya Qur'ani kwa Ibn Hammam, faqihi na msomi mkubwa wa zama hizo. Aidha Shamsud-Din aliandika vitabu kadhaa katika uwanja wa mafundisho ya Kiislamu. Miongoni mwa vitabu vya msomi huyo, ni pamoja na kitabu kiitwacho "Al-taqrir na al-ta'abir."
Na siku kama ya leo miaka 1945 iliyopita Nero, mfalme katili na mmwagaji damu wa Roma alijiua huku akiwa na umri wa miaka 31 na baada ya kutawala kwa miaka 14. Inasemekana kuwa Claudius wa Kwanza wa Roma alimchukua Nero na kumfanya mwanaye. Hata hivyo Nero alimuua Claudius kwa sumu na baadaye kuchukua nafasi yake ya ufalme. Katika kipindi chote cha utawala wake, Nero aliweza kuwaua ndugu na jamaa zake akiwemo mama, mke na kaka yake. Mfalme huyo katili wa Roma alifanya mauaji makubwa dhidi ya wananchi sambamba na kuwauwa kwa halaiki Wakristo na kuuchoma moto mji huo wa Roma, suala lililopelekea kuibuka harakati za uasi dhidi yake. Mtawala huyo katili na dhalimu aliamua kujinyonga baada ya kuona harakati za mwisho za uasi dhidi yake zinakaribia kupata ushindi.

No comments:

Post a Comment